Radio Osotua › Local News

Wizara ya Elimu Yatoa Shilingi Bilioni 22 za Ufadhili wa Masomo

Local News May 21, 2025 John Waicua

Serikali kupitia Wizara ya Elimu imetoa shilingi bilioni 22.03 kugharamia shughuli za masomo kwa muhula wa pili katika shule za umma nchini.

Kulingana na taarifa iliyotolewa na wizara hiyo Jumanne, mgao wa fedha hizo umeelekezwa katika ngazi mbalimbali za elimu ya msingi kama ifuatavyo:

  • Elimu ya msingi bila malipo – Shilingi 1,370,196,684.55

  • Elimu ya shule za sekondari msingi za kutwa – Shilingi 8,900,424,491.35

  • Shule za sekondari msingi zenye mahitaji maalum – Shilingi 118,417,921.35

  • Elimu ya shule za sekondari za kutwa – Shilingi 11,639,872,094.40

Wizara ya Elimu
Taraifa ya Wizara ya elimu kuhusu kutolewa kwa fedha za ufadhili wa masomo

Waziri wa Elimu Julius Ogamba amesema utoaji wa fedha hizo unalenga kuhakikisha kuwa shule zinaendesha shughuli zake bila usumbufu na kwamba wanafunzi wanapata haki yao ya kikatiba ya elimu ya msingi bila malipo.

Aidha, waziri huyo amewaonya walimu wakuu na wakuu wa shule dhidi ya kuwatoza wanafunzi ada au michango yoyote isiyoidhinishwa na serikali, akisema kuwa wizara haitasita kuchukua hatua kali kwa yeyote atakayebainika kutumia vibaya fedha hizo.