Washukiwa Dusit D2

    Familia za watu 21 waliopoteza maisha yao katika shambulizi la kigaidi la Dusit D2 jijini Nairobi mnamo mwaka wa 2019 sasa wamepata nafuu ya haki baada ya washukiwa wawili wa shambulizi hilo kuhukumiwa kifungo cha miaka 30 gerezani kila mmoja.

    Katika uamuzi uliotolewa na Mahakama Kuu jijini Nairobi siku ya Alhamisi, Jaji Diana Kavedza aliwahukumu Mohammed Abdi Ali mwenye umri wa miaka 61 na Hussein Abdile Ali mwenye umri wa miaka 22 baada ya kupatikana na hatia ya kupanga na kufadhili shughuli za kigaidi zilizohusishwa na kundi la Al-Shabaab.

    Kwa mujibu wa uamuzi wa mahakama, ushahidi uliowasilishwa uliweza kuthibitisha kuwa washukiwa walishirikiana kwa karibu na washambulizi waliotekeleza shambulizi hilo lililochukua zaidi ya saa 20, ambapo watu 21 waliuawa, wengine kadhaa kujeruhiwa, na mali kuharibiwa.

    Jaji Kavedza alieleza kuwa vitendo vya ugaidi ni tishio kubwa kwa usalama wa taifa na haki ya kuishi kwa kila raia, na kwa hivyo adhabu hiyo ni onyo kwa wale wanaopanga ama kufadhili vitendo vya kigaidi. Aliongeza kuwa licha ya hukumu hiyo kutoweza kufuta maumivu ya waliopoteza wapendwa wao, ni hatua muhimu ya kuhakikisha haki inatendeka na ya kuwatia moyo manusura pamoja na familia za waathiriwa.

    Familia nyingi zilizokuwa mahakamani wakati wa hukumu hiyo zilionekana kuguswa na hatua hiyo ya mahakama, zikiitaja kama mwanzo wa uponyaji wa kisaikolojia baada ya miaka ya maumivu na kusubiri haki.

    June 19, 2025

    Leave a Comment