Waziri Aden Duale akihutubia Maseneta

Waziri wa Ulinzi Aden Duale amejiwasilisha mbele ya Bunge la Seneti asubuhi ya siku ya Jumatano, ili kujibu maswali mbalimbali kuhusu utendakazi wa Wizara yake. Katika kikao hicho, maseneta walipata nafasi ya kuuliza maswali kuhusu Idara ya Ulinzi wa Taifa, na kwa kiasi kikubwa, shughuli za Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF) nchini Somalia.

Waziri Duale alieleza kwamba jeshi la pamoja linaloendelea na shughuli za kudumisha usalama nchini Somalia litaanza kuondoka mwezi Julai mwaka ujao. Aidha alitoa hakikisho kwamba ifikapo mwisho wa mwaka ujao, kila mwanajeshi wa KDF atakuwa ameondoka kutoka katika taifa hilo.

SOMA PIA :Tutawakabili Alshabaab hadi Mwisho, Waziri wa Ulinzi Aahidi.

Kuhusu hali ya usalama na mahangaiko yanayosababishwa na kundi la Al-Shabaab, Waziri Duale alieleza kwamba jeshi la taifa litaendelea kukabiliana na wanamgambo hao na pia kutoa msaada kwa serikali ya Somalia ili kurejesha amani. Vilevile amesisitiza kwamba usalama wa Somalia ni muhimu sio tu kwa Somalia yenyewe, bali pia kwa ukanda wa Afrika Mashariki na kwa uchumi na ustawi wa eneo hili kwa ujumla.

 

 

October 4, 2023