BY JOHN MSAFIRI

    TUMSIFU YESU KRISTO!

    Majilio ni nini?
    Majilio ni kipindi cha Dominika nne cha kujiandaa na Sherehe ya Kuzaliwa Bwana wetu Yesu Kristo, yaani NOELI.
    Kinawakilisha karne zote za Agano la Kale

    Katika mwaka wa liturujia ya Kanisa katoliki la Roma ,
    sherehe ya Noeli inaandaliwa na kipindi cha
    Majilio ambacho kina mambo mawili:
    kinakumbusha Mwana wa Mungu alivyotujilia
    mara ya kwanza, na papo hapo kinatuandaa
    kumpokea atakapotujilia tena siku ya mwisho . Kwa Maana alisema:
    “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu(Mathayo24:42)

    Kufuatana na hayo kina sehemu mbili: hadi
    tarehe 16 Desemba kinahusu zaidi kurudi kwa
    Bwana; siku nane za mwisho kinatuelekeza
    moja kwa moja kuadhimisha kuzaliwa kwake.
    Urefu wa Majilio unategemea siku
    inayoangukia Noeli, kwa kuwa ni lazima yawe
    na Jumapili nne. Hivyo basi yanaanza kwa
    Masifu ya Jioni ya kwanza ya Jumapili
    inayoangukia tarehe 30 Novemba au tarehe ya
    jirani zaidi; yanakwisha kabla ya Masifu ya
    Jioni ya kwanza ya Noeli.
    Kwa jumla ni kipindi cha toba: rangi yenyewe
    ni zambarau; haziruhusiwi sherehe za fahari;
    ala za muziki na maua vinaweza kutumika
    kwa kiasi tu. Masharti hayo yanalegezwa
    katika Jumapili ya tatu kwa sababu ya furaha
    ya kuona tunakaribia sherehe yenyewe.
    Katika kipindi hicho tunaadhimisha tumaini la
    Israeli lililotimizwa Yesu alipokuja katika
    unyenyekevu wa umbile letu; pia tunangojea
    arudi kwa utukufu. Kama alivyotekeleza ahadi
    mara ya kwanza, atazitekeleza pia mara ya
    pili, ingawa kwake miaka elfu ni kama siku
    moja tu.(Zaburi.90) Kati ya majilio hayo mawili, Bwana
    anatujilia mfululizo kifumbo katika sakramenti
    (hasa ekaristi ) na katika maisha ya kila siku
    kwa njia ya matukio na watu (hasa maskini )

    Basi tunapaswa kuwa tayari daima kumpokea
    ili siku ya mwisho tukamlaki, naye
    atukaribishe kwenye uzima wa milele. Pia
    tunapaswa kumuomba aje kutukomboa, yeye
    aliye tumaini letu.

    Katika safari ya Majilio watu watatu
    wanatuongoza tukutane na Yesu:

    1. Isaya
    Nabii wa tumaini, mwenye kipaji cha kutokeza
    matazamio ya binadamu na kumhakikishia
    atatimiziwa na Mwokozi

    2. Yohane Mbatizaji ,
    mwenye kuhimiza toba kwa kuwa tunapaswa
    kupindua maisha yetu ili tukutane vema na
    Kristo.

    3. Maria , bikira aliyekuwa tayari
    kumpokea Masiya kwa upendo na kushirikiana
    naye katika kutimiza mpango wa wokovu .
    Tukiwafuata hao watatu tunaweza kujipatia
    maadili yale yanayotuandaa kumpokea
    Mwokozi anapotujilia: ndiyo matunda maalumu
    tunayotarajiwa kuyachuma wakati wa Majilio:

    1. Kukesha katika imani, sala na kutambua
    ishara za Bwana kutujilia katika nafasi yoyote
    ya maisha na mwishoni mwa nyakati.

    2. Kuongoka kwa kufuata njia nyofu .

    3. Kushuhudia furaha inayoletwa na Yesu kwa
    kuwa na upole na uvumilivu kwa wenzetu, kwa
    tumaini la kuwa bidii zetu zinawahisha ufalme
    wa Mungu wenye heri isiyo na mwisho.

    4. Kutunza unyenyekevu kwa kufuata mifano ya
    maskini wa Injili ambao ndio waliompokea
    Mkombozi .

    TUMSIFU YESU KRISTO!๐Ÿ‘๐Ÿพ

    November 24, 2022