Rais William Ruto na naibu wake Rigathi Gachagua, wamesema kwamba ukanda wa Nyanza hautaachwa nyuma katika maswala ya maendeleo.

Rais ambaye alikua akizungumza katika eneo la Uriri kaunti ya Migori, katika ziara ya kuzindua miradi ya Maendeleo, alisema kwamba miradi kadhaa iko kwenye mipango ya serikali, na kwamba ushirikiano na viongozi wa eneo hilo utawezesha kukamilika kwa miradi hii ya maendeleo.

Kwa upande wake naibu wa Rais Rigathi Gachagua ametoa wito kwa Rais Ruto kutoiwacha nyuma jamii ya Nyanza katika uongozi wake, na kuihusisha inavyofaa katika kuliendesha taifa. Gachagua alieleza kwamba rais ana jukumu la kuinua jamii ya ukanda wa Nyanza na kuwezesha wananchi wa eneo hilo kujihisi kama sehemu ya serikali ya Kenya kwanza.

Viongozi mbalimbali kutoka eneo la Nyanza walioandamana na Rais wanajumuisha Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia Eliud Owalo(ICT), Waziri wa Elimu Ezekiel Machogu (Elimu), Wabunge Mathias Robi (Kuria Magharibi), Marwa Kitayama (Kuria Mashariki), Mark Nyamita (Uriri) Caroli Omondi (Suba Kusini), Japheth Nyakundi (Kitutu Chache Kaskazini), Elisha Odhiambo (Gem) na Sylvanus Osoro (Mugirango Kusini), Okoth Obado (Aliyekuwa Gavana wa Migori), CAS Fred Outa, Kidero Evans na Nicholas Gumbo miongoni mwa wengine.

March 25, 2023