BY RADIO OSOTUA,9TH DEC,2022-David Wafula Wakoli wa chama cha Ford Kenya ametangazwa mshindi wa kiti cha useneta wa Bungoma.

Uchaguzi mdogo ulifanyika Desemba 8.

Kinyang’anyiro hicho kilivutia wagombeaji 11.

Akizungumza baada ya kumkabidhi Wakoli cheti hicho siku ya Ijumaa, afisa msimamizi wa uchaguzi kaunti ya Bungoma Grace Rono aliwapongeza wawaniaji wote kwa kudumisha amani wakati wote wa kampeni na uchaguzi mdogo.

Nawashukuru wagombea wote waliodumisha amani wakati wa kampeni na siku ya uchaguzi,” alisema.

Wakoli alipata jumla ya kura 66,032, Mwambu Mabonga wa UDA alikuwa wa pili kwa kura 45,901 huku Wafula Wamunyinyi wa DAP-K akipata kura 20,519.

Waliokuwepo wakati wa kukabidhi cheti hicho ni Mbunge wa Kanduyi John Makali, mbunge wa Webuye Mashariki Martin Wanyonyi, Mbunge wa Kwanza Ferdinand Wanyonyi, Balozi Simon Nabukwesi, naibu gavana wa Bungoma Jennifer Mbatiany na kiongozi wa Wengi katika bunge la kaunti ya Bungoma miongoni mwa viongozi wengine.

Wakoli aliwashukuru wakazi kwa kumruhusu kuchukua nafasi ya spika wa bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula kama seneta.

Seneta huyo mteule alimpongeza Wetang’ula kwa kuunga mkono azma yake.

“Wetang’ula alinishika mkono katika maisha yangu yote ya kisiasa. Ninaahidi kuingia na kutenda kama yeye, kuwasilisha masuala na kuwakilisha watu wa Bungoma,” alisema.

Wakoli alisema Wetang’ula alikuwa mchangiaji mijadala mahiri.

Alimpongeza Gavana wa Bungoma Kenneth Lusaka kwa usaidizi wake.

December 9, 2022