Naibu Rais Rigathi Gachagua amekemea Huduma ya Kitaifa ya Polisi kwa kuendeleza shuguli za kufurushwa kwa karibu familia 105 kutoka kwa kipande cha ardhi ambacho walikuwa wamekimiliki kinyume cha sheria katika kijiji cha Kiriko, Rongai, Kaunti ya Nakuru.

Akizungumza mjini Nakuru alipoongoza ugawaji wa chakula cha msaada katika eneo hilo, Gachagua alibainisha kuwa polisi wamepewa mamlaka na sheria kulinda maisha na mali ya Wakenya na wala si kuangalia upande mwingine mali inapoharibiwa.

Kulingana na Gachagua, kabla ya kuwafurusha familia hizo, polisi walipaswa kujadiliana kuhusu njia za kuwahamisha kwa muda katika misingi mipya.

Aliongeza kuwa kamanda wa polisi aliyeongoza oparesheni hiyo, Peter Mwanzo, amerudishwa katika makao makuu ya NPS na kwamba serikali itamchukulia hatua.

February 18, 2023