BY ISAYA BURUGU/BBC ,09,NOV 2022-Serikali ya Ufaransa kupitia ubalozi wake jijini Dar Es Salaam imetangaza kutuma kikosi cha maafisa na wataalamu wa uchunguzi na uchambuzi wa masuala ya usalama wa ndege kusaidia uchunguzi wa chanzo cha ajali ya ndege ya Precision Air iliyoanguka Jumapili mjini Bukoba na kuua watu 19 hukuwengine 24 wakiokolewa.

Taarifa ya kutumwa kwa kikosi hicho imetolewa na Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania Nabil Hajlaoui. Wataalamu hao waliwasili jioni ya jana Jumanne.Ndege iliyopata ajali imetengenezwa na kampuni ya ATR ambayo inamilikiwa na makampuni mawili makubwa ambayo ni AIRBUS kutoka Ufaransa na LEONARDO kutoka Italia.

Kampuni ya ATR pia imetuma wataalamu wake nchini Tanzania kusaidia uchunguzi kama inavyotakiwa na sheria za kimataifa za usalama wa anga.Mamlaka za Tanzania awali zilitangaza kuwa hali ya hewa mjini Bukoba ilikuwa mbaya wakati ajali hiyo ikitokea.

Uchunguzi wa kina ulianzishwa toka Jumapili na Serikali ya Tanzania na sasa timu hizo za wataalamu kutoka ng’ambo zinatarajiwa kuupa kasi uchunguzi huo.

 

November 9, 2022