Wizara ya Afya nchini Kenya imetoa wito wa matumizi zaidi ya chanjo ya HPV inayokinga saratani ya mlango wa uzazi kwani ni asilimia 33 tu ya wasichana nchini Kenya wamechanjwa.

Kulingana na Wizara ya Afya, asilimia 61 ya wasichana wenye umri wa kati ya miaka 10 na 14 wamepata dozi ya kwanza ya chanjo hiyo na asilima 31 wamepata dozi ya pili.

Akizungumza wakati wa kongamano la wadau wa saratani ya mlango wa uzazi Dkt.Mary Nyangasi, ameeleza kuwa idadi kubwa ya wanawake walioathiriwa na saratani wanatoka katika familia maskini na pia wana kiwango cha chini cha elimu.

Amesisitiza umuhimu wa wazazi na walezi kuwapeleka watoto wao wa kike kupata chanjo hiyo ya HPV. Wizara  ya afya pia imebainisha kuwa wanawake 9 hufariki kutokana na saratani ya mlango wa uzazi kila siku, na hilo linaweza kuzuiwa kwa kupata chanjo.

Gavana wa Embu Cecily Mbarire kwa uapnde wake ameahidi kuwa bingwa wa saratani katika Baraza la Magavana, na kuwataka wakuu wa kaunti kuzingatia mikakati ya kuzuia ugonjwa huo.

February 28, 2023