Mamlaka Huru ya kutathmini utendakazi wa polisi IPOA imeanzisha uchunguzi baada ya watu sita kuuawa kwa kupigwa risasi wakati umati ulivamia Kituo cha Polisi cha Isebania huko Migori Alhamisi jioni.

Kwa mujibu wa ripoti ya polisi kuhusu tukio hilo, kundi hilo la watu lilifika katika kituo cha polisi kwa gari la kubebea mizigo na kuanza kurusha mapanga na mawe.

Maafisa wa polisi walilazimika kutumia risasi baada ya kundi hilo kuvamia ofisi ya ripoti na ghala la silaha na kuelekea seli ili kuwaachilia wafungwa.

IPOA, katika taarifa kwa vyumba vya habari siku ya Jumamosi, ilisema watu sita walipigwa risasi na kufa wakati wa uvamizi huo wa kutisha na wengine kadhaa kuachwa wakiwa wamejeruhiwa vibaya, miongoni mwao afisa wa polisi.

Mamlaka hiyo ilisema itapendekeza kufunguliwa mashtaka kwa maafisa wowote wa polisi watakaopatikana na hatia ya kutumia vibaya bunduki zao.

May 27, 2023